Newsroom

More on this post

HOTUBA YA DKT. REGINALD MENGI, MWENYEKITI WA TAASISI YA SEKTA BINAFSI TANZANIA KATIKA MKUTANO NA MHESHIMIWA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI NA SEKTA BINAFSI – TAREHE 3 DESEMBA 2015, IKULU, DAR ES SALAA

Mheshimiwa, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;

Mheshimiwa Balozi Ombeni Sefue, Katibu Mkuu Kiongozi;

Wajumbe wa  Baraza la Taifa la Biashara;

Wadau wote wa Sekta Binafsi;

Wageni Waalikwa;

Mabibi na Mabwana:

Mheshimiwa Rais

Kwa niaba yangu binafsi na kwa niaba ya Sekta Binafsi Tanzania nakushukuru sana kwa kutupa fursa ya kukutana nawe katika kipindi kifupi tu baada ya kushika uongozi. Uamuzi huu pekee ni ishara njema kuhusu hekima yako na utayari wako wa kutaka kubadilishana mawazo na wadau wa Sekta Binafsi.

Sekta Binafsi inakupongeza kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Tunaamini kwamba wewe pamoja na Makamu wa Rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan mkishirikiana na Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassim Majaliwa mna nia ya dhati ya kupunguza ama kumaliza kabisa changamoto zinazoikabili jamii ya Watanzania na kuboresha maisha ya wananchi wote.

Kwa niaba ya sekta binafsi hapa nchini, nachukua nafasi hii kusema kuwa tulisikiliza kwa makini hotuba yako wakati unafungua Bunge la 11 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Katika hotuba hiyo tuliona mwanga na kupata matumaini makubwa sana ikiwa ni pamoja na nia yako ya dhati ya kuwakomboa watanzania. Hivyo basi, tunaahidi kushirikiana kikamilifu na serikali yako tukufu katika kuinua uchumi wa Taifa letu.

Pili, tunachukua fursa hii kukupongeza kwa uongozi wako mahiri wa kutaka kuleta mabadiliko katika utendaji na uwajibikaji wa Serikali (Government Delivery).  Tumeshuhudia kwa siku zako hizi chache za uongozi, umeleta mipango mikubwa ya mabadiliko ambayo yanatokea serikalini na kwamba sekta binafsi ina imani chubby na umahiri, uwajibikaji na utendaji wako na imani katika ofisi yako ambayo ni kiungo muhimu kati ya serikali na sekta binafsi.

Mheshimiwa Rais,

Kama sote tunavyofahamu, Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) ni taasisi mwavuli wa asasi za sekta binafsi nchini na lengo lake la msingi ni kutetea sera nzuri na mageuzi muhimu katika kuboresha na kuendeleza mazingira mazuri ya biashara na uwekezaji nchini Tanzania. TPSF inawakilisha sauti ya pamoja wa wadau kutoka sekta zote zinazounda Sekta Binafsi kwa:

a. Kuwa kiunganishi cha sekta binafsi katika maswala ya uraghibishaji katika kuleta maendeleo ya muda mere kwa sekta binafsi nchini Tanzania.

b. Kusimamia na kuhimiza mchakato endelevu wa majadiliano kati ya serikali na sekta binafsi.

c. Kuhimiza ushindani ulio sawa kwa lengo la kukuza shughuli za uzalishaji na biashara kwa lengo la kuinua uchumi wa watanzania kwa jumble

Tunaamini kwamba sekta binafsi Tanzania kupitia taasisi yake ya kitaifa, (TPSF), ina jukumu la msingi la kuhoji, kuchochea, kusimamia na kuimarisha  ukuaji wa uchumi na maendeleo ya kijamii ya taifa letu kwa jumla. Hivyo, tunawajibika kuwa mstari wa mbele katika kuhoji sera za uchumi, kutafiti na kupendekeza sera ambazo tunahisi ni bora zaidi na kushawishi serikali kutekeleza mapendekezo yetu.

Mheshimiwa Rais, katika kipindi kifupi cha siku ishirini na sita tu, tumeshuhudia mageuzi makubwa katika mfumo mzima wa utendaji kazi katika serikali yako.  Tunapata faraja sana na jinsi unavyoyashughulikia mambo mbali mbali yanayokwaza ustawi wa uchumi wetu. Tunakuunga mkono kwa dhati kabisa katika juhudi hizi. Mojawapo ya kero kubwa kwa jamii yetu ni rushwa. Changamoto mbaya kuliko zote ni KUKITHIRI KWA RUSHWA ambayo isipodhibitiwa kwa hakika itakwamisha NDOTO ya nchi hii ya kuhitimu kutoka Taifa lenye kipato cha chini (maskini) hadi kufikia Taifa la kipato cha  kati ifikapo mwaka 2025.

Taarifa ya hivi karibuni ya Afrobarometer na REPOA (Machi 2015) inaonesha kwamba asilimia 71 ya wananchi 2,386 waliohojiwa wanahisi kwamba hakuna utawala bora nchini na kwamba rushwa ilizidi kukithiri mwaka 2014.

Licha ya kwamba sampuli ya utafiti huu ni ndogo bado hoja ya msingi inaonesha asilimia kubwa waliohojiwa wanahisi hakuna utawala bora. Hili umelikemea vikali na kulishughulikia kwa vitendo katika kipindi kifupi tangu ushike madaraka ya Rais. Mheshimiwa Rais, tunasikitika kukuarifu kwamba hata Sekta Binafsi inahusika katika kansa hii mbaya kabisa ya rushwa na Taasisi yetu inawajibika kufanya kazi kubwa zaidi kukabiliana na wafanyabiashara na wawekezaji wasiozingatia maadili.

Tukirejea hotuba yako ya uzinduzi wa Bunge la 11, umesisitiza nia yako ya dhati ya kuunda mahakama  maalum ya kushughulikia mafisadi. Hatua hii  pekee ni miongoni mwa mambo mengi ambayo yanatupa imani kubwa kwa serikali yako. Tunakuahidi chamber tupo pamoja katika vita hii. Hata hivyo, tunaomba tu kwamba misingi ya utawala wa sheria na uhuru wa mahakama vizingatiwe katika maamuzi haya.

Mheshimiwa Rais,

Sekta Binafsi kwa kulingana na Dira ya Maendeleo ya Taifa  (Vision 2025) na Mpango wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini Tanzania (MKUKUTA) ni injini ya kukuza uchumi na hivyo kuwa kichocheo na mhimili muhimu katika maendeleo endelevu na ujenzi wa Taifa.

Sekta hii imekuwa ikitoa mchango mkubwa hususani kupitia wawekezaji na wafanyabiashara katika kukuza ajira, kuleta mapato ya kodi kwa serikali, na kupunguza umaskini unaokadiriwa kufikia asilimia 28.2 ya wananchi wote. Sekta binafsi imekuwa ikitoa mapato ya kodi ya wastani wa shilingi bilioni 800 kila mwezi na kwa mwaka 2014/15, inategemewa kuweza kuchangia takriban shilingi trilioni 11.9 ya bajeti yote ya serikali ambayo ni shilingi trilioni 19.5. Sekta binafsi imetoa ajira rasmi zipatazo 1,233,068 kwa mwaka 2013 pekee kupitia fursa mbalimbali.

Tanzania imeendelea kuongoza kwa kuvutia uwekezaji wa kigeni miongoni mwa nchi za jumuiya ya Afrika Mashariki. Mpaka kufikia mwaka 2013 Tanzania ilikua na thamani ya uwekezaji wa kigeni ufikiao USD 12.7 bilioni ukilinganisha na nchi za Kenya na Uganda zilizokua na thamani ya USD 3.4 bilioni na USD 8.8 bilioni.

Mheshimiwa Rais, uchumi wetu umekuwa ukikabiliwa na changamoto nyingi; ikiwa ni pamoja na urasimu uliokithiri mipaka, utitiri wa kodi na tozo mbalimbali, rushwa katika manunuzi ya umma, matumizi holela yasiyokidhi ukuaji wa mapato ya serikali, sera zisizokuwa na muono mpana na zisizotabirika, miundo mbinu mibovu kama umeme, reli na ufanisi duni wa bandari, huduma duni  za afya na elimu, barabara mbovu za vijijini, riba zilizo juu kwa mitaji ya wajasiriamali wadogo na wale wa kati n.k.

Changamoto hizi zitakwamisha ndoto ya nchi hii kuhitimu kutoka nchi zenye kipato cha chini (maskini) hadi kufikia nchi za uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.

Ili kufikia malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa, hitaji la sekta binafsi iliyo imara na mahiri halikwepeki. Kwa msingi huo tunaomba uongozi wako uweke msukumo tofauti (business unusual) katika maeneo makuu manne yafuatayo:

1. Kuzingatia misingi ya utawala bora hususani katika kupambana na rushwa

Mheshimiwa Rais katika swala la kusimamia misingi ya utawala bora sekta binafsi inaungana na wewe kwani tangu umeapishwa umekua mstari wa mbele kusimamia maadili ya utendaji kazi ikiwemo kuonyesha nia ya dhati ya kudhibiti kero ya rushwa ambayo imekuwa kikwazo kikubwa katika ukuaji wa sekta binafsi na uchumi kwa ujumla..

Katika Swala la kupambana na Rushwa sekta binafsi inapendekeza  kurekebishwa kwa sheria ya Kuzuia na Kupambana na rushwa (The Prevention and Combating of Corruption Act No. 11 of 2007, PCCA No. 11/2007) kwa lengo la kuipa taasisi ya Kuzuia na Kupambana na rushwa (PCCB) mamlaka ya kuchunguza kesi zinazohusiana na rushwa na kuzitolea maamuzi (powers to prosecute).

Kuwepo na uwazi kwenye manunuzi ya umma yanayozingatia thamani ya fedha (value for money), hii  itarahisisha mapambano dhidi ya rushwa, na endapo itabainika watumishi wa umma hawakuzingatia utaratibu huu, hatua za uwajibishwaji zichukuliwe haraka iwezekanavyo.

2. Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi

Mheshimiwa Rais swala la uwezeshaji wananchi kiuchumi ni njia pekee duniani iliyoonesha mafanikio katika kukuza uchumi wa nchi mbalimbali,kupunguza umaskini na kudumisha amani na utulivu.

Tunatambua kuwa serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kuwezesha wananchi kiuchumi lakini tunapendekeza kuwepo kwa sera mtambuka ya ushirikishwaji wananchi (overarching local content policy) katika sekta zote za uchumi.

3. Mazingira wezeshi ya Biashara na Uwekezaji

Tunatambua jitihada mbalimbali zilizofanywa na serikali katika uboreshaji wa mazingira ya ufanyaji biashara na uwekezaji katika kuinua uchumi ili kufikia Malengo ya Dira ya Maendeleo 2025.

Jitihada hizi ni pamoja na kuleta Programu ya Kuboresha Mazingira ya Uwekezaji inayoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu; Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN) unaoratibiwa na Ofisi yako Rais na mipango mingine mingi.

Mheshimiwa Rais, kasi ya utekelezaji wa Mageuzi ya Kisera na Kiutawala ni ndogo sana hapa nchini. Tanzania imeendelea kufanya vibaya na kudorora kwenye ripoti mbalimbali za Kimataifa zinazopima mazingira wezeshi ya biashara na uwekezaji kama World Bank Doing Business Reports ambapo kwa mwaka huu Tanzania imeshika nafasi ya 139 kati ya nchi 189 zinazofanyiwa tathmini duniani.

Mheshimiwa Rais, tunatambua kuwa ili nchi yeyote iendelee ni lazima wananchi wake walipe kodi kulingana na sheria na taratibu zilizowekwa katika nchi husika. Hivyo basi sekta binafsi Tanzania iko tayari kushirikiana na serikali yako kuhakikisha kodi zote stahiki zinalipwa. Ni jukumu letu sote kuhakikisha kwamba tunatekeleza wajibu wetu na pia tunaiomba serikali kuweka mazingira wezeshi.

Katika uboreshaji wa mazingira ya biashara sekta binafsi inapendekeza serikali kuendelea kupitia kwa kina taratibu na sheria za ulipaji kodi kwani kuna biashara ambazo zimelazimika kufungwa na nyingine zipo hatarini kufungwa kutokana na kuzidiwa na mlolongo wa kodi. Mheshiwa Rais mfano wa kodi na tozo ambazo zimekuwa kikwazo kikubwa katika kuleta maendeleo ya sekta mbalimbali za uchumi ni pamoja na tozo na kodi katika usafiri wa anga ambapo kuna tozo zaidi ya 155, kwenye kilimo kuna tozo zaidi ya 100, nakadhalika.

Mheshimiwa Rais tunaamini kuwa serikali yako kwa kushirikiana bega kwa bega na sekta binafsi itafanikiwa kupatia ufumbuzi  maeneo mbalimbali yaliyoainishwa kukwamisha ufanyaji wa biashara hapa nchini, hii ni pamoja na kuwa na mtazamo wa kibiashara katika nyanja zote za kiuchumi ikiwa nipamoja na uboreshwaji sera,mikakati ya nchi na kutokomeza urasimu ili kuweza  kuvutia wawekezaji wa ndani na wa nje.

Mheshimiwa Rais, tunaamini kuwa Serikali yako kwa kushirikiana bega kwa bega na sekta binafsi itafanikiwa kupatia ufumbuzi maeneo mbalimbali yaliyoanishwa kukwamisha ufanyaji wa biashara hapa nchini,hii ni pamoja na kuwa na mtazamo wa kibiashara katika nyanja zote za kiuchumi ikiwa ni pamoja na uboreshwaji sera,mikakati ya Nchi na kutokomeza urasimu ili kuweza kuvutia wawekezaji wa ndani na nje.

4. Mageuzi thabiti ya sekta ya kilimo nchini

Mheshimiwa Rais, inafahamiaka kuwa sekta ya Kilimo ni muhimili mkuu wa uchumi wa Tanzania. Takribani asilimia 75 ya Watanzania wanaishi sehemu za vijijini ambako shughuli zao kuu ni kilimo, ufugaji na uvuvi.

Pamoja na sekta ya kilimo kuajiri watanzania walio wengi sekta hii inakabiliwa na changamoto mbalimbali zinazokwamisha ukuaji wake, zikiwemo upatikanaji wa ardhi iliyotengwa na kurasimishwa kwa ajili ya kilimo cha mazao na ufugaji, upatikanaji na matumizi ya pembejeo za kilimo, kilimo ambacho bado kinategemea mvua, ukosefu wa mikopo, matumizi madogo sana ya zana za kisasa, mazao yetu kuuzwa yakiwa ghafi, upatikanaji na matumizi ya pembejeo za kilimo,kilimo ambacho bado kinategemea mvua,ukosefu wa mikopo matumizi madogo sana ya zana za kisasa,mazao yetu kuuzwa yakiwa ghafi,upatikanaji mdogo wa masoko ya mazao, upotevu wa mazao baada ya mavuno, kodi zilizokithiri, kukosekana kwa taarifa za bei ya mazao ambazo ni sahihi na kwa haraka na kutoimarika kwa vyama vya ushirika.

Pamoja na mafanikio yaliyopatikana, kuna changamoto kadhaa kwa sekta binafsi na serikali ambazo zinatarajiwa kutatuliwa kupitia TNBC.

Kwanza, gharama za kufanya biashara Tanzania zinaendelea kuongezeka. Kwa mfano, Benki ya Dunia imetoa ripoti ya hali ya kufanya biashara kwa mwaka 2013; Tanzania imeshika nafasi ya 134 kati ya  nchi 185 ikilinganishwa na nafasi ya mwaka jana ya 133 kati ya nchi 185 mwaka 2012.  Ripoti inaendekea kuonyesha kwamba Tanzania imefanya vibaya katika maeneo ya 11 yaliyofanyiwa tathmini:-  kuanzisha biashara, kupatikana kwa vibali vya ujenzi, kupata huduma za umeme, kusajili mali, kupata mikopo , kulinda wawekezaji, kulipa kodi, kufanya biashara ya kuvuka mipaka, kutekeleza mikataba, kutatua ufilisi na kuajiri wafanyakazi.

Pili, tumeshika nafasi ya chini kama nchi yenye uwezo mdogo wa ushindani (Low Competitiveness Potential country). Kwa taarifa zilizoandaliwa na Jukwaa la Uchumi Duniani (WEF), Tanzania mwaka huu imeshuka zaidi kwa nafasi tano katika Ushindani (Global Competitiveness Index). Tanzania ilishika nafasi ya 125 mwaka 2013/14 ikilinganishwa na nafasi ya 120 mwaka 2012/13 kati ya nchi 148 zilizofanyiwa utafiti.

Rushwa, miundombinu duni hasa barabara zetu na mitandao ya reli, upatikanaji wa nishati hasa ya umeme, ugumu wa kupata mikopo ni miongoni mwa changamoto na vizuizi kwa wawekezaji wengi. Sababu nyingine ni pamoja na rasilimali watu hawajaandaliwa kielimu au mafunzo ya kitaalamu ikiwemo maadili hafifu ya utendaji kazi na teknolojia duni.

Mheshimiwa Rais,

Njia sahihi ya kujenga uchumi ulio imara na endelevu ni kuwawezesha watanzania wote kwa nafasi walizonazo kushiriki katika ujenzi wa uchumi na Taifa letu. Hii haimanishi Tanzania isivutie wawekezaji kutoka nje.Wanahitajika. Ni suala la uwiano mzuri.

Nakutakia kila la heri na Baraka zake Mwenyezi Mungu katika maisha yako na kukuahidi tena kuwa tutashirikiana kulisukuma gurudumu la maendeleo ya Taifa letu.

Asante sana!

Posted on
Posted in Dr R. Mengi