Newsroom

More on this post

Mengi azindua shindano la 3N – ‘Nitabuni wazo la biashara, Nitatekeleza, na Nitafanikiwa’

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

Dar es salaam:                                                                   8 Januari, 2014.

 

Katika kuendeleza jitihada zake za miaka mingi za kuwashawishi na kuwahamasisha  Watanzania kujiamini kuwa kwa kutumia nguvu na maarifa wanaweza kujikwamua na umaskini kwa kubuni na kuendesha wenyewe miradi ya ujasiriamali, Mwenyekiti Mtendaji wa IPP, Dk Reginald Mengi, kwa mara nyingine amezindua Shindano la kubuni Wazo la Biashara liitwalo ambapo jumla ya shilingi milioni 60 zitashindaniwa.

 

Shindano hilo jipya lijulikanalo kwa kifupi – 3N-ikiwa ni kifupisho cha  ‘Nitabuni wazo la Biashara, Nitatekeleza, na Nitafanikiwa”,  litakuwa linafanyika kila mwezi kwa muda wa miezi sita kuanzia Januari Mosi 2015, hadi Juni 30, 2015, na  mshindi wa kila mwezi atajishindia  ruzuku ya shilingi milioni 10 atakazozitumia kutekeleza kwa vitendo wazo lake la biashara.

 

Shindano hilo, litakalowashirikisha Watanzania pekee, litaendeshwa kwa njia ya mtandao wa kompyuta ambapo mshiriki atatuma wazo lake la biashara kwa anuani ya twita @regmengi Shindano la Wazo la Biashara, na mshiriki anashauriwa kutuma zaidi ya wazo moja, na mshindi wa kila mwezi atachaguliwa na jopo la Wataalamu baada ya kujiridhisha kuwa amekidhi vigezo vya kuwa ni wazo bora Zaidi kwa mwezi huo.

 

Jopo la wataalamu litapitia mawazo yote yatakayowasilishwa, na  kuchagua mawazo 10 bora zaidi, na kabla ya kumpata mshindi, Jopo hilo la Wataalamu litawahoji kwa njia ya simu washiriki hao 10 watakaopita  mchujo huo wa kwanza, ili lijiridhishe kama mawazo  waliyoyatuma ni yao binafsi, na kama wamejipanga vizuri kuyatekeleza kibiashara.

 

Hii ni mara ya tatu kwa Dkt. Mengi kuendesha shindano kwa kutumia mtandao wa kompyuta wa twita kwa kuamini kwake kwamba  mitandao ya kijamii ina nguvu kubwa  katika kuchochea ujasiriamali hasa kwa kizazi cha sasa.

 

Shindano la kwanza na la pili lililoendeshwa mwaka jana lilikusudiwa kushawishi mawazo ya kuondoa umaskini katika taifa lenye utajiri mkubwa, lakini watu wake wengi wakiwa bado wametopea katika lindi la umaskini.

 

Akizungumza katika uzinduzi huo Dkt. Mengi alisema shindano hilo limelenga kuhimiza watu kuwa na upeo mkubwa wa kuona fursa za kibiashara na kuzitumia kujikwamua kiuchumi. Pia alisema   shindano hilo ni mchango wake binafsi wa kuunga mkono jitihada za serikali na sekta binafsi za kuwakomboa wananchi kiuchumi kwa njia za ujasirimali, kwani amesema Sera zote mbili za kitaifa za Elimu ya juu na maendeleo ya viwanda vya kati na vidogo zina vipengele vya  kuchochea na kuendeleza utamaduni wa ujasirimali wa mtu mmoja mmoja.

 

“Kwa muda mrefu nimekuwa nikishawishi uwepo wa moyo wa ujasirimali miongoni mwa wa Watanzania na hasa kwa vijana. Ni ndoto yangu kuona  uchumi wetu unakua kwa kasi kiasi cha kuzalisha zaidi ya mamilionea 100 kila mwaka  wanaoendesha biashara halali,” alisema.

 

Alisema kuwa na wazo sahihi la biashara, katika muda muafaka na eneo sahihi ni muhimu zaidi kuliko ruzuku ya fedha.

 

“Nataka vijana watambue kwamba wanaweza kuanza na kitu kidogo na kukua kufikia kampuni kubwa kabisa ya kimataifa unayoweza kufikiria,” alisema na kusisitiza kwamba anaamini siku moja mazingira ya ujasirimali nchini Tanzania yakuwa miongoni mwa mazingira bora kabisa barani Afrika.

 

Amesisitiza kuwa Shindano hilo liko wazi kwa watanzania wote  na wanachotakiwa kufanya ni kuhakikisha wanapeleka wazo lao la biashara kwa Dk Mengi kupitia mtandao wa kompyuta wa twita, kwa kumtag Dk Mengi kwenye @regmengi.

 

Aidha amesema ni wale tu watakaomtag ndio watafikiriwa na jopo la  wataalamu, na kusisitiza kuwa maamuzi ya jopo la Wataalamu yatakuwa ni ya mwisho.

 

Washindi wa kila mwezi wataarifiwa kwa kutumiwa ujumbe mfupi kwa kupitia akaunti zao za twita (DM) na kupewa ruzuku yao katika sherehe fupi itakayohudhuriwa na waandishi wa habari.

Posted on
Posted in Dr R. Mengi